Wednesday 10 June 2020

Uganda yaandaa hospitali ya wazi yenye vitanda 40,000


Rais wa Uganda anataka wajiandae kwa ongezeko la maambukizi

Rais wa Uganda Yoweri Museveni amesema nchi hiyo inaandaa hospitali ya sehemu ya wazi yenye vitanda 40,000 katika uwanja wa michezo wa Namboole uliopo mji mkuu, Kampala kwa ajili ya wagonjwa wenye virusi vya korona

Rais huyo amesema wizara ya Afya awali ilipanga kuweka vitanda 9,000 lakini aliagiza idadi hiyo iongezwe.

Uganda mpaka sasa ina idadi ya watu 657 wenye Covid-19, ugonjwa unaoathiri pumzi unaosababishwa na virusi vya korona.

Bw Museveni alisema nchi hiyo imefanikiwa kuzuia vifo vinavyohusiana na virusi vya korona lakini akaonya kwamba idadi inavyoongezeka na vifo vinaweza kutokea.

Alisema ili kuzuia maambukizi ya virusi hivyo miongoni mwa jamii, watu wanatakiwa kuwa makini zaidi na kukaa nyumbani kama hawana jambo la muhimu la kufanya.

Chanzo: BBC

Tuesday 9 June 2020

Kiongozi wa upinzani Tanzania atarajiwa kupelekwa Dar


Kiongozi wa Chadema Freeman Mbowe (katikati) anaendelea na matibabu hospitali

Kiongozi wa upinzani Tanzania, Freeman Mbowe ameshambuliwa na kujeruhiwa na watu wasiojulikana kwenye mji mkuu Dodoma.

Msemaji wa chama chake cha Chadema amethibitisha tukio hilo kwa Idhaa ya Kiswahili ya BBC.

Amesema kiongozi huyo wa chama alikuwa akirejea nyumbani kwake siku ya Jumatatu washambuliaji walipomvamia na kumjeruhi mguu.

Mnadhimu mkuu wa upinzani Ester Bulaya alisema kuna mipango inafanyika kumsafirisha Mbowe kwa njia ya anga na kumpeleka jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi kutokana na shambulio hilo.

Viongozi mbalimbali wamemtembelea kiongozi huyo hospitalini akiwemo Naibu Spika, Dr.Tulia Ackson na Spika wa Bunge la Tanzania Job Ndugai.

Kulingana na mbunge wa Iringa mjini Peter Msigwa, alikuwepo nyumbani kwa mwenyekiti huyo jana jioni pamoja na Godbless Lema, Joseph Mbilinyi na John Heche.

Chanzo: BBC na https://bit.ly/3cOuOx7

Ongezeko kubwa la vifo Nigeria lahusishwa na Covid-19



Vifo vingi Kano vilitokea nyumbani



Waziri wa Afya wa Nigeria Osagie Ehanire amesema 60% ya takriban vifo 1000 visivyoelezeka katika jimbo la kaskazini la Kano huenda vilitokana na Covid-19.

Kundi moja la utafiti lilikubaliana hivyo baada ya kufanya uchunguzi wa ongezeko kubwa la vifo katika jimbo la Kano mwezi Aprili na mapema mwezi Mei- hasa miongoni mwa wazee ambao walikuwa na magonjwa mengine hatarishi.

Baadhi walifariki dunia hospitalini lakini zaidi ya nusu walikufa nyumbani.

Kumekuwa na vifo vengine vingi kama hivyo visivyoelezeka katika majimbo mengine kaskazini mwa Nigeria.

Watu wachache wakiendelea kupimwa katika nchi yenye idadi kubwa ya watu barani Afrika, wataalamu wanahofia virusi hivyo vinaweza vikawa vinasambaa bila kutambuliwa Nigeria.

Mpaka sasa idadi ya watu wenye virusi vya corona vilivyothibitishwa ni 2,801 na vifo 361.

Chanzo:BBC

Friday 5 June 2020

Waziri afukuzwa kwa kutaka kununua pipi za dola mil 2.2

Rais wa Madagascar Andry Rajoelina

Waziri wa elimu wa Madagascar kafukuzwa kazi kutokana na mpango wake wa kuagiza pipi zenye thamani.

Rijasoa Andriamanana alisema wiki iliyopita alikuwa akiagiza pipi hizo kwa ajili ya watoto ili kutuliza ladha “chungu” ya dawa asili ya Covid, kulingana na shirika la habari la AFP.

Covid-Organics ni kitulizo kinachotumia mmea kinachopigwa chapuo na serikali ya nchi hiyo kama tiba ya Covid-19.

Kila mwanafunzi nchini humo alitarajiwa kupewa pipi tatu, kulingana na AFP.

Vyombo vya habari vya ndani vimesema waziri huyo alisimamisha mpango huo baada ya Rais Andry Rajoelina kukataa.

Kufukuzwa kwa waziri huyo kulitangazwa siku ya Alhamisi katika taarifa iliyosema mwenzake kwenye wizara ya elimu, Elia BĂ©atrice Assoumacou, atakaimu nafasi yake.

Ushawahi Kubaguliwa? 'Zoom na Zoo' yajadili hayo



Gumzo katika 'Zoom na Zoo'. Kutokana na ghasia zinazoendelea nchini Marekani baada dunia 

kushuhudia namna George Floyd alivyouawa na polisi kufuatia kukamatwa na kukandamizwa 

shingoni hadi pumzi zikakata, mjadala kuhusu ubaguzi wa rangi umeibuka tena. Zuhura Yunus 

kazungumza na Dan Nkurlu akiwa Marekani, Najma Said -Ujerumani, Muhammed Omar- Uingereza 

na Salim Kikeke- Uingereza. wakieleza uhalisia wa ubaguzi.



Thursday 4 June 2020

James Mattis: Aliyekuwa waziri wa ulinzi wa Trump ahamaki

Image shows U.S. President Donald Trump and former Defence Secretary James Mattis
James Mattis alikuwa waziri wa ulinzi wa kwanza wa Rais Trump - ila alijiuzulu mwaka 2018

Aliyekuwa waziri wa ulinzi wa Marekani James Mattis amemkosoa Rais Donald Trump hadharani, akisema anaigawanya nchi kwa makusudi.

Alisema “alikuwa na hasira na kushangazwa” ya namna Bw Trump alivyokuwa akishughulikia maandamano yanayoendelea juu ya kifo cha Mmarekani mweusi George Floyd mikononi mwa polisi.

Bw Mattis amekosoa vikali “utumiaji mbaya madaraka” ya Bw Trump na kuwaunga mkono waandamanaji wanaotaka kuhakikisha maadili ya Marekani yanazingatiwa, kama ilivyokuwa kwa Rais mstaafu Barack Obama.

Bw Trump amemwelezea Bw Mattis kama “jenerali anayekuzwa kuliko anavyostahili”

Bw Mattis aliachia ngazi mwaka 2018 baada ya Bw Trump kuamua kuondosha majeshi ya Marekani nchini Syria.

Alikuwa kimya muda wote mpaka alipoamua kumtolea uvivu Bw Trump kupitia jarida la Atlantic.

Katika kujibu mashambulio, Bw Trump aliandika mfululizo wa ujumbe kupitia ukurasa wake wa twitter akidai kuwa alimfukuza kazi Bw Mattis.

"Sikupenda “uongozi wake” mtindo wake au hata yeye mwenyewe, na wengi wanakubaliana na hilo," aliandika. "Nashkuru aliondoka!"

Chanzo:BBC


Covid-19: Watafiti Kenya watambua ‘aina tofauti’ za virusi

Getty images


Watafiti Kenya wametambua takriban aina tofauti tisa za virusi vya Covid-19 vilivyosambaa nchini humo katika jitihada za kufuatilia kubadilika kwa virusi hivyo.

Aina hizo 9 hazina tofauti na zile ambazo zimesambaa duniani kote.

Kundi la wanasayansi limetathmini mfumo wa jeni 122 kutoka kwa wagonjwa wenye dalili zilizo dhahiri na kwa wale ambao hazionyeshi licha ya kuwa wameathirika katika mji mkuu, Nairobi, na mjini Mombasa.

"Utafiti huo unaonyesha kuwa maambukizi yaliyogunduliwa na kuthibitishwa Machi 2020 zaidi ni kuwa virusi hivyo vimetokana na watu kutoka nje ya nchi, “ imesema ripoti hiyo iliyotolewa na Taasisi ya Utafiti wa Tiba Kenya (Kemri)

Sampuli zote zilichukuliwa kwa watu nchini Kenya baina ya tarehe 12 Machi hadi Mei 25.

Chanzo: BBC

Wednesday 3 June 2020

Marekani yatoa tahadhari nyingine Tanzania kuhusu Covid-19

Mara ya mwisho kutolewa idadi ya watu walioambukizwa virusi vya korona Tanzania ni Aprili 29


Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania umetoa ushauri mwengine wa tahadhari kwa raia wake wa Marekani kuhusu maambukizi ya virusi vya korona nchini humo.

Katika taarifa walioitia, ubalozi huo ulisema kuwa hatari ya kuweza kuambukizwa virusi hivyo jijini Dar es Salaam, bado ni kubwa, lakini haukutoa ushahidi wowote wa kuthibitisha madai hayo.

Taarifa hiyo imependekeza raia wake waepuke msongamano na wasitoke majumbani mwao.

Ushauri huo unatolewa siku chache baada ya wizara ya mambo ya nje ya Tanzania kumwita kaimu balozi wa Marekani, Inmi Patterson, kupinga ushauri wa safari uliotolewa na ubalozi huo mwezi uliopita ambao unalingana na huu wa sasa.

Kwa taarifa zaidi, bonyeza link ifuatayo https://bbc.in/2U0Ey0L

Naibu gavana wa jimbo la Bauchi, Nigeria apatwa na Covid-19


Baba Tela, the Deputy Governor of Bauchi State
Baba Tela, Naibu gavana wa jimbo la Bauchi

Naibu gavana wa jimbo lililopo kaskazini- magharibi mwa jimbo la Bauchi amepima na kukutwa na maambukizi ya virusi vya corona.

Afisa wa shirika la habari alisema Baba Tela amejitenga kwa sasa na watu wote waliomkaribia wakati hao wamechukuliwa vipimo vyao.

Inadhaniwa kuwa naibu gavana huyo aliambukizwa virusi hivyo wakati akifanya kazi kama mwenyekiti wa kikosi kazi kinachosimamia masuala ya virusi vya korona, kulingana na taarifa iliyotolewa na serikali.

Alishaonyesha dalili ya kuambukizwa virusi hivyo kabla ya kuchukuliwa vipimo hivyo.

Jimbo hilo limethibitishwa kuwa na watu 241 wenye maambukizi ya virusi hivyo kati ya takriban watu 10,000 walioambukizwa nchini humo.

Chanzo: BBC

Tuesday 2 June 2020

Hofu ya maambukizi yasimamisha shule kufunguliwa Uganda


Serikali itaendelea na mpango wake wa kusambaza chakula cha msaada


Rais wa Uganda Yoweri Museveni ameahirisha hatua ya kufungua shule upya kwa wanaomaliza mwaka wao wa mwisho. Amesogeza muda kwa mwezi mmoja zaidi.

Kiongozi huyo alisema kufungua shule upya ni hatari kwani nchi hiyo haina vifaa vya kupimia wanafunzi kila baada ya wiki mbili.

Rais Museveni alisema televisheni mbili zitagaiwa katika kila kijiji kuruhusu wanafunzi kuendelea kujifunza kupitia masomo yanayotolewa kwenye televisheni.

Wakati huo huo, bodaboda bado haziruhusiwi kubeba abiria lakini zinaweza kusafirisha bidhaa.

Makanisa, misikiti, baa, majumba ya starehe na sehemu za kufanyia mazoezi zitaendelea kufungwa kwa siku nyingine 21.

Maduka yameruhusiwa kufunguliwa ilimradi tu yahakikishe wateja wanakaa umbali wa mita 2 kila mmoja.

Kwa taarifa zaidi bonyeza link ifuatayo https://bbc.in/2MrNisl

Monday 1 June 2020

VIRUSI VYA CORONA: SHULE ZAFUNGULIWA ENGLAND ILA WAZAZI BADO WANA MASHAKA


first day back at school
Wazazi wakirejesha watoto wao shuleni huko Norfolk, leo Jumatatu



Wanafunzi wa shule za msingi katika baadhi ya shule England wanarejea- lakini utafiti waonyesha nusu ya wazazi huenda wamewabakiza watoto wao nyumbani.

Kuna hisia tofauti kufuatia shule hizo kufunguliwa upya, hata hivyo katika baadhi ya maeneo shule zitaendela kufungwa.

Watoto kutoka darasa la kwanza hadi la 6 ndio wanaoweza kurejea shuleni, wengi wao ambao hawakwenda darasani kwa wiki 10.

Hatua hii inachukuliwa huku masharti ya kujifungia ndani ‘lockdown’ yakilegezwa, ikiwemo ruhusa ya watu sita kwa pamoja kuweza kukutana katika mazingira ya nje.

Kwa maelezo zaidi bonyeza link ifuatayo https://bbc.in/3cmtfpR




Thursday 2 April 2015

KATIBA MPYA TZ: HAKUNA KURA YA MAONI APRILI 30

Mwenyekiti wa Nec Jaji Mstaafu Damian Lubuva

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imekubali kuahirisha upigiaji Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa iliyopangwa kufanyika Aprili 30, mwaka huu kutokana na kutokamilika kwa uandikishaji wa Daftrai la kudumu la wapiga kura kwa kutumia teknolojia ya Biometric Voters Registration (BVR).

Hatua hiyo inakuja baada ya kuwepo mfululizo wa matamko na ushauri kutoka kwa wadau mbalimbali wa demokrasia kwamba zoezi hilo lisingewezekana kwa sasa hasa kutokana kusuasua kwa mwenendo wa BVR.

Mwenyekiti wa Nec Jaji Mstaafu Damian Lubuva aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo kuwa kazi ya uboreshaji daftari la wapiga kura ni ya msingi kabla ya taratibu zote za upigaji kura.

Jaji Lubuva aliyeonekana kuwa mpole zaidi, alisema kwa uzoefu walioupata Njombe, zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura bado halijakamilika katika mkoa huo na mingine iliyosalia.

“Hivyo tume haitaweza kuendelea na zoezi la upigaji kura ya maoni na zoezi hilo lililotangazwa hapo awali kufanyika Aprili 30, 2015 limeahirishwa hadi tarehe itakapotangazwa na Nec baada ya kushauriana na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar,” alisema Jaji Lubuva.

Kwa nyakati tofauti, vyama vya siasa, asasi za kiraia, taasisi za kidini na wananchi wamekuwa wakiishauri Nec kuahirisha Kura ya Maoni huku vyama vya siasa vikimtaka Rais Jakaya Kikwete atii makubaliano yaliyofikiwa na Kituo cha Demokrasia (TCD) mwaka jana ya kuahirisha zoezi hilo hadi baada ya Uchaguzi mkuu.

Jaji Lubuva alisema kuwa tume yake inaendelea kuboresha daftari la wapiga kura nchi nzima ambapo wanatarajia kukamilisha ifikapo Julai mwaka huu. Nec ilieleza kuwa baada ya kumaliza uandikishaji mkoani Njombe watahamia mikoa ya Ruvuma, Lindi, Mtwara na Iringa.

Chanzo: mwananchi.co.tz

SHAMBULIO LA CHUO KIKUU KENYA 'LAUA 147'



A Kenyan soldier escorts a woman after she was rescued

Idadi ya watu waliouawa katika shambulio lililofanywa na al-Shabab kwenye chuo kikuu kaskazini-mashariki mwa Kenya imeongezeka kufikia 147, maafisa wa serikali walisema.

Harakati za kijeshi za kudhibiti chuo kikuu cha Garissa sasa zimekwisha, huku washambuliaji wote wanne wakiwa wameuawa, walisema.

Maafisa walisema wanafunzi 587 walitolewa, 79 wakiwa wamejeruhiwa.

Sheria ya kupigwa marufuku kutoka usiku inatekelezwa katika baadhi ya sehemu nchini humo.

Kaunti nne katika mpaka wa Kenya-Somalia, Garissa, Wajir, Mandera na Tana River, wamezuia watu kutoka nje siku nzima.

Wanafunzi tisa waliojeruhiwa vibaya sana walisafirishwa kwa ndege kwenye mji mkuu Nairobi kwa matibabu.

Kwa maelezo zaidi, bonyeza link ifuatayo
http://bbc.in/1DrBXQW

CHUO KIKUU KENYA CHASHAMBULIWA



Map showing Garissa in Kenya

Watu wenye silaha waliovaa barakoa wamevamia chuo kikuu kimoja karibu na mpaka wa Somalia kaskazini-mashariki mwa Kenya, wakiua watu wawili na kujeruhi takriban 30.

Majeshi yamezunguka chuo kikuu cha Garissa na kujaribu kupambana na washambuliaji.

Walioshuhudia walizungumzia watu hao wenye silaha wakifyatua risasi ovyo bila kujali ni nani na hivyo kuhofiwa kuwa idadi ya waliokufa inaweza kuongezeka.

Haiko wazi nani anahusika na shambulio hilo, lakini wapiganaji wa al-Shabab wamekuwa wakiishambulia Kenya mara kwa mara.

Garissa na maeneo mengine ya mpakani yamekuwa yakishambuliwa mara nyingi.

Tuesday 31 March 2015

MUHAMMADU BUHARI ASHINDA NIGERIA



File photo: Goodluck Jonathan (left) and Muhammadu Buhari shake hands after signing a peace deal agreeing to respect the outcome of the polls
Goodluck Jonathan (kushoto) na Muhammadu Buhari walikubaliana wiki iliyopita kuheshimu matokeo ya uchaguzi

Aliyekuwa kiongozi wa kijeshi Muhammadu Buhari amekuwa mgombea wa kwanza wa upinzani kushinda uchaguzi wa urais Nigeria.

Chama cha Jenerali Buhari kimesema mpinzani wake, Goodluck Jonathan, alikubali kushindwa na kumpa pongezi.

Bw Jonathan alipishana na Jenerali Buhari kwa takriban kura milioni mbili alipogoma mara ya kwanza kukubali kushindwa.

Waangalizi kwa ujumla wameusifia uchaguzi lakini kumekuwa na madai ya udanganayifu, ambao baadhi wanahofia kunaweza kusababisha maandamano na ghasia.

Kwa taarifa zaidi, bonyeza link ifuatayo

http://www.bbc.co.uk/news/world-africa-32139858

BUHARI 'ANAONEKANA' KUONGOZA UCHAGUZI NIGERIA



People watch election news coverage on television at a street in Lagos, Nigeria, 30 March 2015

Matokeo ambayo bado hayajakamilika kutoka uchaguzi wa Nigeria unaashiria aliyekuwa kiongozi wa kijeshi Muhammadu Buhari amepata kura zaidi kuliko rais wa sasa aliye madarakani, Goodluck Jonathan.

Hata hivyo, majimbo yenye watu wengi zaidi kama vile Lagos na Rivers bado matokeo hayakutangazwa rasmi.

Huku nusu tu ya majimbo ya Nigeria yakiwa yametangazwa, chama cha Jenerali Buhari cha All Progressives Congress (APC) kiliripotiwa kuwa na kura zaidi kwa milioni mbili.

Matokeo zaidi yanatarajiwa kutangazwa siku ya Jumanne.

Tume ya uchaguzi ya Nigeria (Inec) ilisitisha kutangaza matokeo Jumatatu usiku, baada ya kutoa matokeo ya majimbo 18 na mji mkuu Abuja.

Chama cha Rais Jonathan cha People's Democratic Party (PDP) kilipata kura 6,488,210 na cha APC cha Jenerali Buhari kimepata kura 8,520,436.