Tuesday 2 December 2014

HIV 'YAPUNGUA MAKALI'



HIV

Virusi vya HIV vinaanza kupungua makali, kulingana na utafiti mkubwa wa kisayansi.

Watafiti kutoka chuo kikuu cha Oxford kinaonyesha virusi hivyo “vinafubazwa” huku vikiendana na mfumo wa kinga wa miili yetu.

Utafiti huo unasema maambukizi ya HIV yanachukua muda mrefu zaidi kusababisha Ukimwi na mabadiliko ya virusi huenda ikasaidia jitihada za kuzuia kusambaa kwa maradhi hayo.

Baadhi ya wataalamu wa virusi wanapendekeza virusi hivyo mwisho “vitakuwa havina athari yoyote” kwa jinsi vinavyoendelea kuwepo.

Zaid ya watu milioni 35 duniani wameathirika na virusi vya HIV na ndani ya miili yao mapambano makali huwepo baina ya mfumo wa kinga na virusi hivyo.

AL-SHABAB YAUA TENA KENYA


Protests in Nairobi, 25 November 2014
Maandamano makubwa yalifanyika wiki iliyopita kufuatia shambulio katika basi karibu na eneo hilo hilo

Wapiganaji wa Al-Shabab wamewaua watu 36 wengi wakiwa Wakristo wanaofanya kazi kwenye machimbo karibu na mji wa Mandera kaskazini mwa nchi ya Kenya.

Washambuliaji hao wenye makao makuu yao Somalia waliwatenganisha Waislamu na wasio waislamu na kuwapiga risasi za kichwa Wakristo, kulingana na wakazi wa eneo hilo.

Awali, mtu mmoja aliuawa katika baa maarufu kwa wasio Waislamu kwenye wilaya jirani.

Al-Shabab iliwaua watu 28 katika shambulio la basi lililowalenga wasio waislamu katika eneo hilo hilo wiki iliyopita.

Shambulio kwa wachimbaji hao lilifanyika siku ya Jumanne.

Walioshuhudia walisema watu hao walikamatwa saa sita za usiku, wakiwa wamelala kwenye maturubali katika machimbo hayo.

Shambulio hilo lilifanyika ormey, kilomita 15 kutoka mji wa Mandera.

Mtu mmoja aliyetembelea eneo hilo aliiambia BBC baadhi ya waliouawa inaonyesha kama walilazwa chini, na kupigwa risasi kichwani.

Wengine wanahisi maturubali ya wafanyakazi hao yalimiminiwa risasi.

Al-shabab imesema imehusika na mauaji hayo.

                                                                                                   

Monday 1 December 2014

MUHAMMAD: MAARUFU KWA WATOTO WA KIUME, UK



Muhammad limekuwa jina maarufu kwa watoto wa kiume nchini Uingereza, mtandao wa BabyCentre umedai.

Wakati huohuo majina ya kiarabu yamezidi kutumika zaidi.

Vipindi vya televisheni kama vile Game of Thrones pia vimechangia sana kutoa majina ya kizazi kijacho.

Orodha ya majina 100 bora ya watoto kwa mwaka 2014 imeonyesha Muhammad imepanda nafasi zaidi ya 27 kutoka mwaka jana hadi kufika namba moja.

Jina hilo limepata nafasi hiyo baada ya kuchaguliwa na watu 56,157 wa wanachama wa mtandao wa BabyCentre.co.uk waliojifungua mwaka 2014.

Kwa ujumla kumekuwa na ongezeko kubwa la majina ya kiarabu, huku Nur likiwa jipya kuingia katika orodha hiyo katika majina 100 bora ya kike, likiruka hadi nafasi ya 29, na Maryam likipanda mara 59 na kuchukua nafasi ya 35.

Omar, Ali na Ibrahim ni majina mapya kuingia katika 100 bora za kiume.

Sophia ndio namba moja katika majina ya watoto wa kike, na kupata umaarufu tena katika orodha ya mtandao wa BabyCentre nchini Marekani, Brazil, Hispania na Urusi mwaka jana.

Lakini jina linalotamba zaidi upande wa watoto wa kike ni Maryam, huku majina mapya zaidi ni Nur, Emilia na Gracie.

Chanzo: www.theguardian.com

HOTELI CHINI YA BAHARI KISIWANI PEMBA, TANZANIA

   
Ushawahi kufikiria kulala na samaki? Au kuzungukwa na samaki. Hoteli ya kwanza chini ya maji barani Afrika imefunguliwa kisiwani Pemba nchini Tanzania. Hoteli hiyo ina umbali wa mita 250 kutoka baharini. Salim Kikeke katika matangazo ya BBC Dira ya Dunia anasimulia akiwa kisiwani humo.

NDOA YA WATU WENGI KWA MPIGO YAFUNGWA BRAZIL



Mass wedding in Rio de Janeiro

Takriban wapendanao 2,000 nchini Brazil wameoana katika eneo moja mjini Rio de Janeiro, kwenye harusi kubwa ya watu wengi kwa pamoja iliyoweka historia mjini humo.

Tukio hilo la kila mwaka, linalopigiwa chapuo na mamlaka za eneo hilo, lina nia ya kusaidia wapendanao wenye kipato kidogo wasio na uwezo wa kulipia gharama za harusi.


Mamlaka za Rio zilikodisha treni maalum kwa ajili ya wapendanao hao na wageni wao waalikwa.

Takriban watu 12,000 walihudhuria shughuli hiyo katika uwanja wa Maracanazinho.

Majaji walijitolea kuidhinisha shughuli hiyo.



Mass wedding in Rio de Janeiro
Watarajiwa wenye kipato cha dola 640 kwa mwezi waliruhusiwa kufungishwa ndoa kwenye shughuli hiyo 

Wapendanao hao pia walifungishwa ndoa iliyobarikiwa na askofu wa Kikatoliki na padri pia.

Tukio hilo limepewa jina la Dia do Sim", au "Siku ya Nakubali” yaani “I Do Day".

Wengi walioozeshwa walikuwa wakikaa pamoja kwa muda mrefu.

Bw Moraes amekuwa na Ana Rosangela Azevedo,mwenye umri wa miaka 31, tangu mwaka  2010 na mapema mwaka huu waliamua kuhalalisha mahusiano yao.