Monday 27 October 2014

BINTI AJIRUSHA GHOROFANI BAADA YA KUTAPELIWA



Workers House nchini Uganda

Mwanamke mmoja amejirusha kutoka ghorofa ya 14 katika jumba liitwalo Workers House nchini Uganda na kufa baada ya kugundua ‘kaingizwa mjini’ alipokuwa akipeleka pesa nyumbani wakati akifanya kazi Dubai.

Annet Ashaba, mwenye umri wa miaka 26, kutoka wilaya ya Sembabule, alirejea Oktoba 16 na kugundua alitapeliwa fedha zake alizotuma kwa ndugu yake Uganda kumjengea nyumba.

 “...ndugu zake walituambia alituma pesa kwa shemeji yake mmoja kumnunulia kiwanja na baadae akatuma ziada kwaajili ya ujenzi. Lakini Ashaba aliporejea alikuta kiwanja kimenunuliwa lakini nyumba iliyojengwa siyo aliyotegemea,” alisema msemaji wa polisi wa Kampala Patrick Onyango.

Alisema ndugu zake Ashaba aliwaonya kuwa jambo baya linaweza kumtokea.

“Alipofika ghorofa ya 14, alifunga mdomo wake kwa kitambaa halafu akaruka,” Bw Onyango alisema.

Ashaba si wa kwanza kujirusha kutoka Workers House. Septemba 2009, Baker Kilenzi, mwenye umri wa miaka 23, alikata shingo yake mwenyewe kwenye ghorofa ya nane baada ya kuachana na mpenzi wake.

Wiki hiyohiyo, Moses Siraji, mwenye miaka 24, akifanya kazi kwenye kampuni ya mafuta, alijirusha kutoka ghorofa ya 14 na kufa.

Mwaka 2012, binti mmoja aliyehitimu chuo kikuu alijirusha na kufariki dunia baada ya miaka mingi ya kusaka ajira bila mafanikio.

Chanzo: monitor.co.ug 
Imetafsiriwa na Mwandishi wetu

No comments:

Post a Comment