Wednesday 29 October 2014

RAIS WA ZAMBIA AFARIKI DUNIA LONDON



Rais wa Zambia Micahel Sata afariki dunia akiwa madarakani

Rais wa Zambia Michael Sata amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 77 baada ya kupata matibabu ya ugonjwa ambao haujaelezwa hadharani, serikali imesema.

Rais Sata, ambaye alikuwa akipata matibabu Uingereza, amefariki mjini London katika hospitali ya King Edward VII siku ya Jumanne usiku.

Vyombo vya habari vinasema alifariki dunia baada ya “mapigo ya moyo ghafla kwenda kasi”

Haijawekwa wazi bado nani atamrithi Rais huyo. Uamuzi huo unaweza kuchukuliwa na baraza la mawaziri la Zambia linalokutana Jumatano asubuhi.

“Ni kwa moyo mzito sana natangaza kifo cha rais wetu mpendwa,” kiongozi wa mawaziri Roland Msiska alisema kupitia televisheni ya taifa.

Alisema mke wa Bw Sata na mtoto wake wa kiume walikuwa naye alipofariki dunia.

“Nawasihi nyote muwe na utulivu, umoja na amani wakati wa kipindi hichi kigumu,” Bw Msiska aliongeza.

Kifo cha Rais huyo kinatokea siku chache tu baada ya Zambia kusherehekea maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru kutoka Uingereza.

'Mfalme Cobra'

Mapema mwezi huu ripoti kutoka Zambia zilizema Rais Sata alikwenda nje ya nchi kufanyiwa matibabu huku kukiwa na hisia nzito kuwa anaumwa sana.

Baada ya kuondoka nchini, waziri wa ulinzi Edgar Lungu alitangazwa kuwa kaimu Rais.

Makamu wa Rais Guy Scott amekuwa akishika nafasi hiyo mara kwa mara katika matukio rasmi. Lakini ana asili ya Scotland na wazazi wake hawakuzaliwa Zambia, kwahiyo inaweza ikawa kikwazo kikatiba ya yeye kugombea nafasi hiyo.

Akijulikana kama “King Cobra” kutokana na ulimi wake mkali, Bw Sata alichaguliwa kuwa rais mwaka 2011.

Ilikuwa ni nadra kuonekana hadharani tangu kurejea kwenye mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa mwezi uliopita, ambapo alishindwa kuhutubia kama ratiba ilivyopangwa.

Bw Sata Septemba 2011, alimshinda rais aliyekuwa madarakani Rupiah Banda ambaye chama chake kilikuwa madarakani kwa miaka 20.

Chanzo: BBC                         
Imetafsiriwa na Mwandishi wetu



No comments:

Post a Comment