Sunday 4 January 2015

MSANII WA HIP HOP PROF J KUWANIA UBUNGE MIKUMI

 

MKONGWE wa muziki wa kizazi kipya, Joseph Haule ‘Profesa Jay’, anatarajia kugombea Ubunge jimbo la Mikumi Mkoani Morogoro mwaka huu.

Akizungumza na Tanzania Daima, rafiki yake wa karibu na Profesa Jay, Selemani Msindi ‘Afande Sele’, alisema kwa sasa yupo Mikumi kwa ajili ya kumsaidia Profesa Jay katika maandalizi ya uchaguzi mkuu hapo mwakani.

“Nipo na Profesa tunawapigia kampeni wenyeviti wa mitaa na vitongoji katika uchaguzi unaoendelea, kwasababu tukiamini kwamba serikali na msingi mzuri wa uongozi inabidi uanzie chini.

Ina maana nyumba ambayo itakuwa na msingi mzuri ni nyumba bora zaidi. “Kwahiyo tupo hapa Mikumi tukijaaliwa uzima Profesa Jay mwakani ametangaza nia ya kugombea ubunge hapa nyumbani kwao.

Tumeanza kujenga mazingira kwenye uongozi wa chini ili mwakani Profesa akute kuna misingi imara na apate ubunge wa hapa Mikumi, kwahiyo yeye atagombea Mikumi na mimi nitagombea Morogoro mjini kwetu,” alisema.

Aliongeza kuwa, Mikumi ndipo kwao kabisa na Profesa Jay ambaye anatarajia kugombea ubunge kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA), na wameamua kuingia kwenye siasa kwasababu wameshafanya sana nyimbo za kiharakati, wameshaongea mengi kupitia muziki wao lakini bahati mbaya viongozi wamekuwa na masikio magumu.

No comments:

Post a Comment