Sunday 4 January 2015

MSHUKIWA WA MAUAJI AHISIWA KUWA TANZANIA

   
Almahri anasakwa kwa kuhusika na kifo cha Nadine



Msako wa kimataifa unafanyika baada ya mwanamke mmoja kukutwa amekufa kwenye chumba cha hoteli.

Mwili wa Nadine Aburas, mwenye umri wa miaka 28, ulikutwa na wafanyakazi katika hoteli ya Future Inn hotel huko Cardiff siku ya mwaka mpya.

Polisi wa South Wales walisema wanaichukulia kesi hiyo kuwa ya mauaji na wanataka kumsaka mshukiwa Sammy Almahri, raia wa Marekani kutoka mjini New York.

Almahri, mwenye umri wa miaka 44, ambaye ana majeraha yanayoonekana usoni, alikuwa na “urafiki” na Bi Aburas na inaaminiwa kwamba sasa yupo Tanzania, jeshi hilo la polisi limesema.

Mshukiwa huyo aliingia katika hoteli hiyo ya Future Inn hotel huko Cardiff Bay, Desemba 30 kabla Bi Aburas kuwasili kwenye saa tatu usiku.

Halafu aliondoka kwenye hoteli hiyo kwenye saa 9 alfajir siku ya Mwaka mpya na kusafiri kwa ndege kutoka uwanja wa ndege wa Heathrow, Uingereza na kuelekea Bahrain saa nne unusu asubuhi.

Mpelelezi wa polisi Paul Hurley alisema Almahri anachukuliwa kuwa mtu "hatari" na "mwenye mengi" alipozungumza na umma kusaidia kumpata.

Alisema: "Hoteli ilikuwa imeshughulika na watu waliokuwa wakisherehekea Krismasi na Mwaka Mpya. Watakuwepo watu waliowaona pamoja, au peke yao, na ninawasihi wajitokeze.

"Wakati bado hatujakamata mtu yeyote, tuna maafisa wanaojaribu kumsaka Sammy Almahri, ambapo sasa tunaamini yupo nchini Tanzania.

"Tumekuwa tukifanya kazi kwa karibu na wafanyakazi wenzetu wa Marekani na maafisa polisi wa Tanzania.

Kutokana na uchunguzi wetu tumegundua  Almahri ni mtu anayejiweza sana na uwezo wa kupata fedha nyingi, ambayo inaweza kumsaidia kukwepa mkono wa sheria.

Uchunguzi wa mwili wa marehemu umekamilika lakini sababu ya kifo chake bado hakijathibitishwa.

Familia ya Bi Aburas imetoa rambirambi kwake kwa kusema "mzuri, mchangamfu, wa kipekee na mwenye kipaji".

Katika taarifa walisema: "Alikuwa anapenda sana kusaidia watu na kila mtu alimpenda. Ameacha pengo kubwa kwenye familia yetu na kila mmoja anampenda. Familia imeomba waachwe waomboleze kimya kimya.”

Chanzo: www.uk.news.yahoo.com
Imetafsiriwa na Mwandishi wetu




No comments:

Post a Comment