Monday 22 December 2014

ESCROW YAMTOA PROF TIBAIJUKA, MUHONGO KIPORO



Rais wa Jamhuri wa Tanzania Jakaya Kikwete ametangaza kutengua uteuzi wa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka baada ya vyombo vya Serikali kubaini na kijiridhisha kuwa amekiuka maadili ya utumishi wa Umma kwa kuingiziwa fedha kiasi cha Sh1.65bilioni kwenye akaunti yake binafsi.

Rais Kikwete ametangaza kufukuzwa kazi kwa waziri huyo leo alipokuwa anazungumza na wazee wa mkoa wa Dar es Salaam katika Ukumbi wa Diamond Jubilee jijini hapa, na baada ya kutangaza kufukuzwa kwake maelfu ya wazee waliohudhuria kwenye mkutano huo walipiga kelele za kumpongeza Rais Kikwete kwa uamuzi wake.

Rais kikwete amesema miongoni mwa mapendekezo ya Bunge kuhusiana na sakata la uchotwaji wa fedha kwenye akaunti ya Escrow Tegeta yaliyofikishwa kwenye Serikali ni pamoja na kuwajibishwa kwa Bodi ya Shirika la umeme (Tanesco), Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Eliakim Maswi, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Profesa Anna Tibaijuka, pamoja na Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo.

Rais Kikwete amesema baada ya uchunguzi wa vyombo husika viliweza kubaini kuwa kiasi cha Sh1.65bilioni kiliingizwa kwenye akaunti binafsi ya Profesa Tibaijuka, jambo ambalo ni kinyume na maadili ya utumishi wa Umma.

“Tumezungumza na Profesa Tibaijuka na tumemuomba atupishe ili tuweze kuteua waziri mwingine kwani viashiri vyote vinaonyesha kuwa alikiuka kanuni na sheria ya maadili ya Umma,” anasema Rais Kikwete.

Aidha Rais Kikwete amesema katika suala la Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo analiweka kiporo maana bado hajapata ufafanuzi kuhusu mambo kadha wa kadha, hivyo pindi atakapopata ufafanuzi na kujiridhisha ataujulisha umma .

Amesema kuhusu suala la bodi ya Tanesco hana shida nalo kwa sababu tayari bodi hiyo imeshamaliza muda wake hivyo ni kama imekwishajifuta yenyewe, na kuongeza kuwa tayari Ikulu imeshapewa taarifa za kumtaka achague bodi nyingine, hivyo ndani ya siku chache bodi mpya ya Tanesco itatangazwa.

Amesema suala la Katibu Mkuu wa Nishati na Madini na viongozi wengine wa utumishi wa Umma ambao wametajwa katika sakata hilo tume ya maadili, Taasisi ya Kuzuia na Kupapambana Rushwa (Takukuru) pamoja na jeshi la polisi wanaendelea kufanya uchunguzi wao, na ikithibitika kuwa walikiuka maadili yao ya kazi sheria stahiki zitachukuliwa.

Chanzo: mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment