Monday 29 December 2014

MARUBANI WA AIR TANZANIA WAWAACHA ABIRIA 'MABOYA'


 map

Zaidi ya abiria 100 wamekwama katika uwanja wa ndege nchini Tanzania kufuatia marubani kushindwa kuripoti kazini baada ya mapumziko ya Krismasi, maafisa walisema. 

Walitaka wawe wamesafiri Desemba 27 kutoka Dar es Salaam hadi visiwa vya Comoro na maeneo mengine.

Abiria wenye hasira walililaumu shirika la ndege linalomilikiwa na serikali ya nchi hiyo, Air Tanzania, kwa kutowahudumia uzuri.

Msemaji wa Air Tanzania alisema shirika hilo halijui kwanini marubani hao hawakuripoti kazini.

Marubani hao walipewa nafasi ya kupumzika siku ya Krismasi na siku iliyofuata na kutarajiwa kurejea kazini Jumamosi.

"Tunahisi huenda kukawa na tatizo kwasababu hili si jambo la kawaida ," alisema msemaji huyo, Lily Fungamtama.

"Tunaomba radhi kwa abiria wetu wote kutokana na hali hii na tumefanya kila liwezekanalo kuwatafutia ndege mbadala," aliongeza.

Abiria mmoja aliiambia BBC hana uhakika tena kama anaweza kuliamini shirika hilo, kwani limekuwa mara kwa mara likivunja ahadi zake ya lini ndege hiyo itaondoka.

Abiria waliokuwa wasafiri kuelekea katika miji ya Kigoma, kaskazini- magharibi mwa nchi hiyo na 
 Mtwara uliopo kusini wamekwama, pamoja na wale waliokuwa wakielekea visiwa vya Comoro.

Mwandishi wa BBC alisema abiria, wakiwemo wanawake na watoto, wamepewa malazi katika hotel ndogo ndani na maeneo mengine ya mji wa Dar es Salaam.

 

No comments:

Post a Comment