Friday 14 November 2014

BURKINA FASO WAKUBALIANA SERIKALI YA MPITO



Talks on the transition in Ouagadougou. 13 Nov 2014

Utaratibu wa serikali ya mpito nchini Burkina Faso umekubalika baada ya kuwepo mazungumzo baina ya viongozi wa kisiasa, kijeshi na kiraia.

Msemaji wa mazungumzo hayo mjini Ouagadougou alisema makubaliano hayo yamekubalika bila kupingwa.

Serikali hiyo ya mpito inatarajia kurejesha nchi katika uongozi wa kiraia na kuandaa uchaguzi mwakani.

Jeshi lilichukua madaraka baada ya Rais Blaise Comapore alipolazimishwa kujiuzulu tarehe 31 Oktoba kufuatia maandamano mazito.

Lt Kanali Isaac Zida alijitangaza kuwa mkuu wa taifa hilo la Afrika magharibi tarehe 1 Novemba kufuatia Rais Compaore kukimbilia nchi jirani ya Ivory Coast baada ya kukaa madarakani kwa miaka 27.

Kulingana na azimio walilokubaliana siku ya Alhamis, rais wa mpito atachaguliwa na kundi maalum litakalohusisha viongozi wa kidini, kijeshi, kisiasa na kitamaduni.

Baada ya hapo rais atamtaja waziri mkuu atatakayeteua  wanachama 25 wa serikali.

Azimio hilo pia limetoa wito wa kuwepo wanachama 90 wa baraza la kitaifa la mpito kuhudumu kama bunge.

Lt Kanali Zida, aliyeahidi kukabidhi madaraka kwa raia, anatarajiwa kutii azimio hilo kwa siku chache zijazo, maafisa walisema.

Chanzo: BBC
Imetafsiriwa na Mwandishi wetu

No comments:

Post a Comment