Saturday 15 November 2014

RAIS BOUTEFLIKA 'ALAZWA UFARANSA'



 Abdelaziz Bouteflika
Rais wa Algeria Abdelaziz Bouteflika amelazwa katika hospitali moja nchini Ufaransa, kulingana na maafisa wa Ufaransa.

Kiongozi huyo, aliyepooza mwaka jana, kwa sasa anatibiwa Grenoble, vyanzo vya polisi na serikali vimesema.

Maafisa hao hawakutoa maelezo zaidi kuhusu afya ya Bw Bouteflika.

Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 77 ameiongoza Algeria tangu mwaka 1999, na amekuwa akionekana hadharani kwa nadra sana tangu kuchaguliwa kwake tena kwa mara ya nne mwezi Aprili.

Bw Bouteflika alilazwa hospitalini siku ya Alhamis, kulingana na maafisa wa Ufaransa waliotaka majina yao yahifadhiwe.

'Si kweli'

Gazeti la Ufaransa la Le Dauphine Libere limesema Bw Bouteflika alilazwa kwenye wodi ya masuala ya moyo katika hospitali binafsi kwenye mji ulio kusini-mashariki mwa Ufaransa.

Gazeti hilo liliripoti kuwa ghorofa nzima aliopo yeye lililipiwa ili kuhakikisha kuna usalama wa kutosha.

Serikali ya Algeria haijasema lolote kuhusiana na taarifa hizo za kulazwa kwa rais.

Hatahivyo, mkuu wa chama tawala FLN alisema taarifa hizo “si za kweli”, shirika la habari la Reuters lilisema.

No comments:

Post a Comment