Sunday 14 September 2014

'MAUAJI' MENGINE KUFANYWA NA IS YACHUNGUZWA

David Haines
Bw Haines alitekwanyara mwaka jana alipokuwa akitoa misaada Syria

Wizara ya mambo ya nje ya Uingereza imesema " inafanya kazi haraka iwezekanavyo kuthibitisha"  video inayodai kuonyesha kukatwa kichwa kwa mateka ambaye ni raia wa Uingereza, David Haines.

Wizara hiyo imesema kama ni kweli ni "mauaji ya kukera", na wakati huohuo wanaendelea kushirikiana na familia ya Bw Haines.

Mfanyakazi wa shirika moja la kutoa misaada, mwenye umri wa miaka 44, kutoka Perth, alitekwa mwaka jana nchini Syria.

Wapiganaji wa kundi la Islamic State IS tayari wamewakata vichwa waandishi wawili wa habari wa Marekani na kutishia kumwuua Bw Haines iwapo mashambulio ya anga ya Marekani nchini Iraq hayatositishwa.

Bw Haines, baba wa watoto wawili, alichukuliwa mateka katika kijiji cha Atmeh, jimbo la Idlib nchini Syria, mwezi Machi 2013.

Alikuwa akilisaidia shirika la Kifaransa la kutoa misaada Acted, baada ya kufanya hivyo hapo awali nchini Libya na Sudan kusini.

Tukio hilo limetokea saa chache baada ya familia yake kuliomba kundi la IS moja kwa moja kuwasiliana nao siku ya Ijumaa.

Video hiyo inaonyesha pia tishio la kumwuua mateka mwengine Mwingereza.

Waziri mkuu wa Uingereza David Cameron amesema tukio hilo "ni la kukera mno na la kutisha"

"Ni tukio la ukatili wa hali ya juu. Ninawapa pole familia ya David Haines walioonyesha ujasiri wa ajabu mpaka sasa na wakati wote tangu alipotekwa.

"Tutafanya kila liwezekanalo ndani ya uwezo wetu kuwasaka wauaji hawa na kuhakikisha haki inatendeka, hata iwe kwa muda gani," alisema.

Msemaji wa serikali ya Uingereza alisema waziri mkuu huyo ataitisha mkutano wa dharura baadae hii leo.

Chanzo: BBC
Imetafsiriwa na Mwandishi wetu

No comments:

Post a Comment